Shughuli ya kupiga kura nchini Afrika ya Kusini ilianza vyema mapema leo asubuhi huku idadi kubwa ya wapigaji kura ikijitokeza.
Zaidi ya watu milioni 25 nchini humo hii leo
wamepanga foleni katika vituo vya upigaji kura kwa uchaguzi mkuu wa mara
ya tano tangu kumalizika kwa utawala wa enzi ya ubaguzi wa rangi.Wapiga kura wamekuwa wakituma ujumbe kwenye Twitter na Facebook wakilalamika kuhusu muda mrefu wa kusubiri kabla ya kupiga kura katika moja ya vituo vya kupigia kura eneo la Lonehill.
Baadhi wamesema wamesubiri kwa saa tano kabla ya kupiga kura kwa sababu ya foleni ndefu.
Huu ni uchaguzi wa kwanza kufanyika tangu kutokea kifo cha hayati Nelson Mandela, aliyekuwa rais wa kwanza mweusi wa Afrika Kusini.
Uchaguzi umefanyika bila matatizo yoyote huku wapiga kura wakiwa na furaha wakijipanga kupiga kura hasa miongoni mwa wapiga kura wageni.
Chama tawala cha African National Congress, ANC ndicho kilicho maarufu zaidi. Lakini umaarufu wa chama hicho na rais Jacob Zuma umeathirika kutokana na tuhuma za rushwa na matatizo ya kijamii.
Licha ya kukumbwa na kashfa za ufisadi na utawala mbovu, duru zinasema kuwa chama cha ANC huenda kikanyakuwa ushindi kwa mara nyingine.
Uchaguzi huo unasimamiwa na maafisa zaidi ya 200,000 wa tume ya uchaguzi watakao zunguka mikoa yote 9 iliyoko nchini humo.
Mwandishi wa BBC mjini Johannesburg anasema kuwa raia wengi wa Afrika Kusini bado wanakipenda chama cha ANC,kwa sababu kimeweza kuweka udhibiti na kujali masilahi ya wananchi masikini.
Anasema kuwa kifo cha Nelson Mandela huenda kimeipa ushaiwishi mkubwa chama hicho.
No comments:
Post a Comment