Polisi nchini Kenya wamesema kuwa wamewakamata
washukiwa wawili wa mashambulizi yaliyofanyika mjini Mpeketoni, Pwani ya
Kenya na kusababisha vifo vya zaidi ya watu 60.
Kundi la wapiganaji wa Al Shabaab limekiri
kufanya mashambulizi hayo yaliyofanyika Jumapili usiku na Jumatatu usiku
ingawa serikali ya Kenya imesema kuwa mashambulizi hayo yalichochewa
kisiasa.''Tumewakamata watu kadhaa kuhusiana na mashambulizi ya Mpeketoni, akiwemo miliki wa gari moja lililotumika katika mashambulizi hayo,'' alinukuliwa akisema mkuu wa polisi David Kimaiyo.
Mshukiwa wa pili aliyekuwa anaandika kwenye akaunti ya Twitter inayoshukiwa kumilikiwa na Al Shabaab pia alikamatwa. Anadaiwa kutangaza kuwa Al Shabaab ndio waliofanya mashambulizi hayo
Licha ya madai ya haraka kutoka kwa kundi la Al Shabaab kuwa wao ndio waliotekeleza mashambulizi hayo, Rais Uhuru Kenyatta katika hotuba yake kwa taifa alilaumu vikundi vya wanasiasa pamoja na makundi ya watu ambayo yana nia ya kufaidi kutokana na hali mbaya ya usalama nchini humo kwa kufanya mashambulizi hayo.
Maafisa kadhaa wa polisi wa eneo la Mpeketoni, wamefutwa kazi na wengine kuhamishwa kutoka vituo vyao vya kazi katika eneo hilo.
Hii ni baada ya tuhuma dhidi yao kuwa walipuuza onyo la kutokea kwa mashambulizi hayo kutoka kwa shirika la ujasusi. Wanatarajiwa kufikishwa mahakamani kujibu mashitaka.


No comments:
Post a Comment