Tuesday, 27 October 2015

CCM YAIBUKA KIDEDEA JIJINI MWANZA.

Stanslaus Mabula akiongea na wanahabari baada ya kutangazwa mshindi wa Ubunge Jimbo la Nyamagana (CCM)


Mgombea wa Chama cha Mapinduzi CCM Jimbo la Nyamagana Mkoani Mwanza ameibuka mshindi wa kiti cha Ubunge katika jimbo hilo kwa kupata kura 81,017 na hivyo kumbwaga aliyekuwa mbunge wa jimbo hilo Ezekiel Wenje kutoka Chama cha Demokrasia na Maendeleo Chadema aliyepata kura 79,280.
Matokeo hayo yalitangazwa na Msimamizi Mkuu wa Uchaguzi Jimboni humo ambaye pia ni Kaimu Mkurugenzi wa Jiji la Mwanza Tito Mahinya huku kukiwa na Ulinzi Mkali wa vyombo vya ulinzi na usalama katika viunga vya ofisi za Jiji hilo.
Akitakangaza matokeo hayo majira ya saa saba usiku wa kuamkia leo, Mahinya alibainisha kuwa pia CCM imeibuka kidedea kwa upande wa Madiwani ambapo kati ya Kata 18, imeshinda Kata 14 na Chadema Kata Nne.
Msimamizi Mkuu wa Uchaguzi Mwanza Bw,Tito Mahinya akitangaza Matokeo ya Ubunge jimboni humo.

Kwa upande wa Wagombea wengine, Chacha Okong’o (ACT Wazalendo) alipata kura 161, Faida Potea (CUF) amepata kura 1,005, Ahmad Mkangwa (NRA) kura 104, Mohamed Msanya (Jahazi Asilia) kura 175 na Ramadhan Mtoro (UDP) amepata kura 68.
Wanahabari wakijaribu kupata yanayojiri kwa ajili ya kuwajuza wananchi.
Hata hivyo kabla ya matokeo hayo kutangzwa, Mgombea kutoka Chadema Ezekiel Wenje alikataa kusaini karatasi ya wagombea na kubainisha kuwa demokrasia haikutumika katika zoezi zima la uhesabuji wa kura katika uchaguzi huo na kwamba atafuata hatua zaidi za kisheria katika kupinga matokeo hayo.
Kushoto ni Katibu wa CCM Wilaya ya Nyamagana akiwa na Katibu wa CCM Mkoa wa Mwanza Miraji Mtaturu (kulia) muda mfupi kabla ya matokeo kutangazwa
Kwa upande wake Mshindi wa Uchaguzi huo Stanslaus Mabula alisema kuwa tangu awali alitarajia ushindi huo na kwamba suala la demokrasia limezingatiwa. Katika hatua nyingine Mabula alibainisha kuwa atahakikisha anatatua changamoto zinazolikabiri Jiji la Mwanza ikiwa ni pamoja na kuwaunganisha wakazi wa Jiji katika shughuli mbalimbali za uzalishaji ili waweze kujitegemea kiuchumi.
Ezekiel Wenje akiongea na wanahabari muda mfupi kabla ya matokeo kutangazwa.

No comments: