Sunday, 21 February 2016

JECHA:-PAMOJA NA MADAI YA KUJITOA{UCHAGUZI MKUU-ZANZIBAR}BADO TUNAWATAMBUA WAGOMBEA WA VYAMA HIVYO.

Licha ya Chama cha Wananchi (CUF) na vyama vingine sita vya siasa kuandika barua ya kueleza kutoshiriki Uchaguzi Mkuu wa marudio uliopangwa kufanyika Machi 20, mwaka huu, Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar (ZEC), Jecha Salim Jecha amesema ofisi yake bado inawatambua wagombea wa vyama hivyo.“Mgombea Urais wa CUF na wagombea wake wa Baraza la Wawakilishi na Madiwani, na vyama vingine sita waliandika barua kwa ZEC wakisema hawatashiriki uchaguzi huo. Kwa bahati mbaya, wagombea wote na vyama vyao vya siasa vinavyodai kususia, wameshindwa kufuata taratibu.
“Inaelezwa wazi katika Kifungu cha 31 na 37A na Sura ya 46 na 50 ya Sheria ya Uchaguzi ya Zanzibar, kuhusu taratibu za uteuzi wa wagombea na jinsi gani wagombea wanaweza kujitoa katika uchaguzi. Hakuna hata mgombea mmoja aliyefuata sheria hiyo,” alisema Jecha katika taarifa yake kwa vyombo vya habari jana.
Jecha alisema kulingana na kanuni, ni jukumu la chama cha siasa kuandika kwa ZEC kuhusu kuondoa udhamini wake kwa mgombea. Alisema hata CUF ambayo mgombea wake ni Maalim Seif Shariff Hamad, imeshindwa kufuata kanuni hizo.
“Ni muhimu sana kuelewa na kufuata sheria za uchaguzi. Tumekuwa tukiwasiliana na vyama vyote 14 vya siasa, sambamba na kusambaza vifaa vya uchaguzi kwa wilaya zote kumi na moja kabla ya kuvitawanya baadaye kwenye vituo 1,580 vya kupigia kura,” alisema Jecha.

No comments: